24/04/2024
DEAR PESA
____________
Mpendwa pesa, ni nini nilichokukosea? Mbona umejitenga na kuwa mbali ya upeo wa macho yangu? Niweke wazi ili nielewe.
Labda mimi ndiye mkosefu kwako, lakini mbona kumbukumbu zangu hazioneshi nilichowahi kukukosea.
Iwapo kunalo jambo lililokukera kwangu naomba uliweke wazi nitambue. Mie nikitakacho ni mimi na wewe kumaliza tofauti zetu.
Mwanzo ulipokaa kwangu siku tatu nilidhani huenda ndio umekuja mazima na hautaondoka tena. Kitendo chako cha kuondoka ghafla kiliniletea msongo wa mawazo. Kidogo hata nijinyonge k**a sio huyu jirani yangu kukata kamba. Mimi nililala nilipoamka sikukukuta. Mpaka leo sijajua chanzo ni kipi.
Ni nini ulichoona kibaya kwangu mpendwa pesa mpaka hutaki kurudi?
Au ulishajua kuwa ukiishi kwangu nitabadilika nijae majivuno na dharau. Ama uliona sina sehemu ya kukuhifadhi?
Mpendwa pesa.......
Nimeshapata habari kuwa wanafiki walikujaza maneno eti nimekutukana. Lakini ukweli ni kwamba wala sikukutukana, mimi nilipita tu nikasikia wakikusema vibaya, kuwaβeti wewe pesa ni shetani. Basi mimi nikaamua kukutetea, nikakataa na kukataa kuwa wewe sio shetani bali malaika mwema mtatuzi wa changamoto. Hapo nilifanya makosa?
Mpendwa pesa.. ...
Kila siku naisafi mikono yangu ili angalau siku ukirejea nikushike bila kukuumiza. Labda mikono yangu yenye gaga mithili ya wembe ndiyo unayoihofu. Lakini mbona miezi yakatika pasipo dalili yako?
Ama waleti yangu inatoa harufu mbaya inayokufanya ushindwe kurudi ukiikumbuka? Au ni kadi zangu za benki zisizo hata na ndururu ndizo unaziziogopa huku ukiona utakuwa mpweke kuishi ndani yake?
Mpendwa pesa.......
Mimi bado nakupenda! Ushakwenda tezi na omo, basi rejea ngamani tuanze ukurasa mpya niache kunung'unika.
Au iwapo hutaki kurejea leo mtume hata mwakilishi wako aje kunipooza kwa hizi shida nilizo nazo wakati wewe ukifungasha mafurushi yako ili uje jumla.
Mpendwa pesa.....
Nimekumiss hakika. Siku zote nataabika, Sina hata pa kushika. Hebu rudi malaika, niache kuhangaika! Ukweli wazi naweka, toka ulipoondoka chakula hakijanishuka. Hali yangu ya mashaka, sina shoka wala shuka.
Nipo tayari kukulaki k**a upo warudi. Iwapo kuja hutaki nasema tupo tunaingia site kukutafuta mimi na wanangu. Tumeshajua ulipo.
Marwa